Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Mary Makondo, amesema kifo cha mfanyabiashara maarufu Titho Mbilinyi, anayejulikana zaidi kama Mwilamba, kimeacha pengo kubwa si tu kwa familia yake bali pia kwa jamii nzima na maendeleo ya mkoa wa Ruvuma.
Akitoa salamu za pole kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed nyumbani kwa marehemu Mwilamba mjini Songea, Makondo amesema Mwilamba atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika kuwaunganisha wafanyabiashara, kusimamia masuala ya uchumi, na kushirikiana na serikali katika kuhamasisha uwekezaji na kukuza biashara.
Amesema Mwilamba alikuwa mstari wa mbele kusikiliza changamoto za wafanyabiashara na kuzifikisha katika mamlaka husika, wakati huo huo akisisitiza mshikamano na ushirikiano wa kweli kati ya serikali na sekta binafsi.
Makondo amesisitiza kuwa jamii imepoteza mtu muhimu, kiongozi shupavu na mzalendo wa kweli, hivyo ameihimiza jamii kuenzi mema yote yaliyofanywa na marehemu na kuyatumia kama dira ya kuendeleza mshikamano na maendeleo ya pamoja katika mkoa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Ruvuma, Komredi Oddo Mwisho, amesema Mwilamba ni miongoni mwa watu waliotoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa ilani ya chama kupitia huduma alizotoa kwa jamii hususan katika masuala ya kilimo.
Ameeleza kuwa Mwilamba alikuwa akijitahidi kuwasilisha changamoto za wafanyabiashara katika ofisi za chama, kutafuta suluhisho bila kutumia nguvu, na kushirikiana na serikali katika kuwaelimisha na kuwaelekeza wafanyabiashara na kuwafanya wafanyabiashara wa Ruvuma kuwa waungwana na wasikivu licha ya changamoto walizokuwa wakikutana nazo.
Kwa upande wake aliyekuwa Mbunge wa Songea Mjini, Dkt. Damas Ndumbaro, amesema mchango wa mfanyabiashara Mwilamba katika mji wa Songea, mkoa wa Ruvuma na Taifa ni mkubwa na hauwezi kufutika, hivyo ni vema kufuata nyayo zake katika kushirikiana na watu na kuleta maendeleo.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.