PATO la Taifa katika Mkoa wa Ruvuma limeongezeka kutoka shilingi bilioni 2.37 mwaka 2012 hadi kufikia bilioni 6.39 mwaka 2022.
Kwa mujibu wa takwimu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Pato la Taifa (GDP) katika kanda hiyo limekuwa linaongezeka mwaka hadi mwaka na kufanya kanda hiyo kuchangia wastani wa asilimia 10.5 ya Pato la Taifa katika Mkoa wa Ruvuma.
Kwa mujibu wa NBS ongezeko hilo limechangiwa Zaidi na uzalishaji katika shughuli za madini na kilimo
Uzalishaji wa madini ya makaa ya mawe Ruvuma
Uzalishaji wa madini ya makaa ya mawe katika Mkoa wa Ruvuma umekuwa chanzo kikubwa cha mapato ya serikali ambapo katika mwaka wa fedha wa 2023/2024,serikali imeweza kuuza tani 1,356,249.84 za makaa ya mawe zenye thamani ya Dola za Marekani Zaidi ya milioni 144.9.
Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Alphonce Bikulamchi anasema Kupitia mauzo hayo serikali imekusanya kiwango cha mrabaha wa Dola za Marekani 3,937,434.98 na ada ya ukaguzi Dola za Marekani 914,034.68 na kwamba madini hayo yameuzwa ndani ya nchi,nchi Jirani,barani Ulaya na Asia kupitia bandari ya Mtwara na Dar es salaam.
Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2023/2024 Ofisi ya Madini Mkoa wa Ruvuma, ilipangiwa kukusanya jumla ya shilingi bilioni 41 na kwamba katika kipindi cha kuanzia Julai hadi Desemba ofisi hiyo ilikusanya Zaidi ya shilingi bilioni 13 sawa na asilimia 64.
Uchimbaji na uuzaji wa makaa ya mawe mkoani Ruvuma ulianza mwaka 2011 kukiwa na Kampuni moja ya uchimbaji ya Tancoal Energy ambapo hadi kufikia mwaka 2019 wadau wengi walijitokeza na kufanya uwekezaji mkubwa katika uzalishaji wa madini ya makaa ya mawe.
Leseni za Uchimbaji na Biashara ya Madini
Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Ruvuma imekuwa ikitoa leseni mbalimbali za uchimbaji na biashara ya madini kama vile leseni za uchimbaji mdogo (PML), leseni za madini ya biashara (Dealers na Brokers).
Kwa mujibu wa Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Alphonce Bikulamchi kwa kipindi cha mwaka wa fedha wa 2021/2022 hadi 2024/2025, idadi ya leseni zilizotolewa zimekuwa zikiongezeka, huku mkoa ukiwa na jumla ya leseni 144 za utafutaji madini na leseni za uchimbaji mkubwa na wa kati.
Ukusanyaji wa Maduhuli ya Serikali:
Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2024/2025, Ofisi ya Madini Mkoa wa Ruvuma ilikusanya jumla ya shilingi 105,120,541,415.03, sawa na asilimia 126 ya lengo la makusanyo.
“ Huu ni uthibitisho wa ufanisi katika usimamizi wa makusanyo ya fedha zinazotokana na shughuli za madini, ikichangiwa na ongezeko la mauzo ya madini’’,anasema Mhandisi Bikulamchi
Masoko ya Madini:
Mkoa wa Ruvuma unasimamia masoko mawili ya madini ambayo ni Soko la Madini ya Dhahabu na Vito lililopo Songea Mjini, na Soko la Madini ya Vito katika Wilaya ya Tunduru.
Afisa Madini Mkazi Mkazi Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Alphonce Bikulamchi anasema Masoko haya yamesaidia kuimarisha biashara ya madini, na kwa kipindi cha mwaka wa fedha wa 2021/2022 hadi Disemba 2024, jumla ya madini yaliyouzwa katika masoko haya ilikuwa na thamani kubwa, ikiwemo madini ya vito na dhahabu.
Uzalishaji wa Makaa ya Mawe:
Uchimbaji wa makaa ya mawe katika mkoa wa Ruvuma umeongeza kasi tangu mwaka 2011, na kwa mwaka 2021/2022 hadi 2024/2025, ambapo kiasi cha tani 8,848,176.91 za makaa ya mawe kilikuwa kimeuzwa.
Mhandisi Bikulamchi anasema kutokana mauzo hayo Serikali ilikusanya shilingi 78,797,933,654.78 kupitia mrabaha na ada za ukaguzi na kwamba biashara ya makaa ya mawe imechangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa mkoa.
Meneja Uchimbaji wa kampuni ya Mgodi wa Makaa ya Mawe ya JITEGEMEE Wilayani Mbinga Mkoani Ruvuma Bosco Mabena anasema malori zaidi ya 120 hubeba makaa ya mawe kwa siku katika mgodi huo na kwamba uzalishaji wa madini hayo unafanyika kwa njia za kisasa.
Mabena anasema makaa ya mawe yanayozalishwa kwenye mgodi wa Kampuni ya JITEGEMEE hutumika katika viwanda vilivyopo ndani ya nchi,Afrika Mashariki na nchi za Ulaya na China.
“Huu ni mgodi wa kitanzania ambao unaendeshwa na wazawa kwa asilimia 100,tunavyo vitalu vya makaa ya mawe ambavyo vinachimba makaa ya mawe kwa njia ya kisasa kwa sababu tuna vifaa vya kisasa vikiwemo maabara ya kisasa na mitambo ya kuchakata makaa ya mawe kwa ubora wa hali ya juu’’,alisisitiza Mabena.
Anasema makaa ya mawe yanatumika katika viwanda mbalimbali vikiwemo vya saruji katika mikoa mbalimbali nchini,pia amesema makaa ya mawe yanatumika katika viwanda vya tires,nondo na viwanda vyote vidogo vidogo vikiwemo viwanda vya nguo ambapo amesema wanapakia makaa ya mawe bandari ya nchi kavu zaidi ya 120 kwa siku.
Hata hivyo anasema Kampuni ya JITEGEMEE ina ghala la kutunzia makaa ya mawe katika bandari ya Mtwara lenye uwezo wa kutunza makaa ya mawe zaidi ya tani laki tano kwa ajili ya kuuza katika masoko ya nje ya nchi kupitia bandari ya Mtwara.
Mafanikio ya Sekta ya Madini:
Sekta ya madini mkoani Ruvuma imekuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa mkoa na taifa kwa ujumla.
Mhandisi Bikulamchi anayataja baadhi ya mafanikio yaliyopatikana ni pamoja na ongezeko la makusanyo ya maduhuli kutoka wastani wa shilingi bilioni 21.6 mwaka 2021/2022 hadi kufikia shilingi bilioni 30 mwaka 2023/2024.
Anasema kumekuwepo na ongezeko la mauzo ya makaa ya mawe kutoka wastani wa tani 1.5 milioni mwaka 2021/2022 hadi tani 2.56 milioni mwaka 2023/2024 ambapo anasisitiza kuwa hiyo ni ishara ya mafanikio katika sekta hii ambayo inatoa ajira na kuongeza mapato ya serikali.
Sekta ya madini mkoani Ruvuma inaendelea kuimarika na kutoa mchango mkubwa katika uchumi wa mkoa na taifa. Uwekezaji wa ziada, usimamizi mzuri wa masoko, na ongezeko la makusanyo ya maduhuli ni baadhi ya mafanikio yanadhihirisha ukuaji wa sekta hii.
Dhamira ya serikali ya Awamu ya Sita ya kuanzisha masoko ya kisasa ya madini na ongezeko la idadi ya migodi, kunaufanya mkoa wa Ruvuma kuendelea kuwa kivutio kwa wawekezaji hivyo kuwa chanzo muhimu cha mapato kwa serikali.
Biashara ya madini ya makaa ya mawe mkoani Ruvuma ilishamiri baada ya mauzo jumla ya makaa ya mawe ya tani 450,675.32 ndani ya nchi na tani 1,060,699.05 ziliuzwa nje ya nchi katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2022.
Mwaka 2019 wadau wengi walijitokeza na kufanya uwekezaji katika shughuli za Makaa ya Mawe hali iliyosababisha kuongezeka kwa uzalishaji wa madini hayo kuanzia mwaka 2020.
Uzalishaji wa Madini ya Makaa ya Mawe mkoani Ruvuma unatoa mchango mkubwa kwenye maduhuli yanayokusanywa na Tume ya Madini Mkoani Ruvuma.
Katika kipindi cha hivi karibuni, Makaa ya Mawe yamekuwa yakihitajika sana ulimwenguni kama chanzo cha nishati na hivyo kuwa moja ya chanzo kikubwa cha mapato ya Serikali.
Katika Mwaka wa fedha 2021/2022, Ofisi ya Madini Mkoa wa Ruvuma ilipangiwa kukusanya maduhuli ya serikali kiasi cha Shilingi bilioni 12,Hata hivyo hadi kufikia Juni 30,2022, Ofisi ya Madini Ruvuma ilikuwa imekusanya kiasi cha Shilingi Bilioni 21,sawa na asilimia 179 ya lengo la Mwaka huo.
Katika Mwaka wa fedha 2022/2023, Ofisi ya Madini Ruvuma ilipangiwa kukusanya zaidi ya Shilingi Bilioni 26 hadi kufikia Desemba 31,2022,Ofisi ya Madini Ruvuma ifanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 19 sawa na asilimia 75.25 ya lengo.
Madini ya makaa yam awe yanayochimbwa Ruvuma, huuzwa ndani ya nchi, nchi zinazotuzunguka,barani Ulaya na Asia kupitia bandari ya Mtwara na Dar es Salaam.
Shughuli za utafiti wa makaa ya mawe Ruvuma
Shughuli za utafiti na uchimbaji wa makaa ya mawe katika mkoa wa Ruvuma zinafanyika katika Wilaya ya Mbinga maeneo ya Mbalawala,Mbuyula,Paradiso,Ntunduwaro,Amanimakoro na Ngaka, katika Wilaya ya Songea katika maeneo ya Muhukuru, Mdunduwalo,Njuga na kikunja na Wilaya ya Nyasa maeneo ya Malini.
Waziri Mkuu wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa amewahi kutembelea na kukagua mgodi wa makaa ya mawe wa Kampuni ya Jitegemee katika Kijiji cha Ntunduwaro wilayani Mbinga ambapo aliridhishwa kutokana na kushamiri kwa biashara hiyo.
Waziri Mkuu alifurahishwa na biashara ya makaa ya mawe baada ya kutembelea mgodi mmoja tu wa Jitegemee ambapo alielezwa mgodi umetoa ajira za kudumu 85,ajira za muda 150 ambapo alisema hiyo ni faida kubwa kwa wananchi na serikali ambayo inapata mapato makubwa kutokana na kodi na tozo mbalimbali.
Utafiti umebaini kuwa Mkoa wa Ruvuma una hazina ya makaa ya mawe zaidi ya tani milioni 227 ambazo zinatarajiwa kuchimbwa kwa miaka 300.
Utafiti uliofanywa Mwaka 2001,kwenye mgodi wa Ngaka wilayani Mbinga ulibaini kuwepo kwa madini ya makaa ya mawe yanayoongoza kwa ubora duniani kiasi cha tani milioni 400.
Tafiti za awali za makaa ya mawe zimefanyika katika maeneo ya Mbalawala Mbinga ambako imebainika kuwa na tani milioni 99.5, Mbuyula Mbinga tani milioni 15.1 na Muhukuru Songea tani milioni 27.
Utafiti mwingine umefanyika katika eneo la Njuga wilaya ya Songea ambako kuna tani milioni 23, wilaya ya Nyasa maeneo ya Malini kata ya Mtipwili tani milioni 29, kijiji cha Liweta Kata ya Mbaha tani milioni 34.
Ubora wa makaa ya mawe yanayopatikana kwenye maeneo hayo yana wastani wa Calorific Value (CV)5,000 hadi 7,000,hata hivyo uchimbaji mkubwa wa makaa ya mawe unafanyika katika maeneo ya Mbalawala,Mbuyula, Mbambabay, Muhukulu na Liweta.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.