Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, amesema ukuaji wa sekta ya kilimo unakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo upatikanaji wa mitaji, maarifa ya kifedha na uelewa wa namna ya kushirikiana na taasisi za kifedha ili kuongeza uzalishaji.
Ametoa kauli hiyo wakati akifungua mafunzo ya elimu ya kifedha kwa wakulima wa Wilaya ya Songea, yaliyotolewa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) katika ukumbi wa Songea Club, mjini Songea.
Brigedia Jenerali Ahmed amesisitiza kuwa elimu inayotolewa na benki hiyo itawawezesha wakulima wa Ruvuma kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara, na hivyo kuufanya mkoa huo kuwa kinara wa uzalishaji wa chakula nchini.
Kwa upande wake, Afisa Utafiti Mkuu wa TADB, Bw. Chisker Masaki, amesema benki hiyo imebaini kuwa wakulima wengi hawana taarifa sahihi kuhusu fursa zinazotolewa na TADB, hivyo, wameamua kutembelea mikoa na wilaya mbalimbali ili kutoa elimu na kuwahamasisha wakulima kuchangamkia mikopo ya kilimo kwa ajili ya kuinua uzalishaji.
Ameeleza kuwa TADB inatoa mikopo kwa wakulima moja kwa moja kupitia benki hiyo, pamoja na kushirikiana na taasisi nyingine za kifedha kupitia Mfuko wa Dhamana kwa wakulima wadogo. Kupitia mfumo huo, wakulima mmoja mmoja, vikundi vilivyosajiliwa, vyama vya ushirika na kampuni zinazojihusisha na kilimo wanaweza kupata mikopo kwa urahisi.
Naye Afisa Mwandamizi wa Huduma kwa Wateja wa TADB, Bi. Faithful Zion Joshua, amesema hadi sasa benki hiyo imefikia wakulima zaidi ya 2,000 katika mikoa 15 na wilaya takribani 20, ambapo wakulima binafsi, vikundi na vyama vya ushirika wamepata elimu na huduma zinazotolewa na benki hiyo, hatua inayolenga kuimarisha sekta ya kilimo nchini.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.