Jeshi la Polisi mkoa wa Ruvuma linawashikilia watuhumiwa saba baada ya kukamatwa na nyara mbalimbali za wanyamapori zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 314, Nyara hizo ni pamoja na meno ya tembo 64, meno ya kiboko 145 na meno mawili ya ngiri.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma SACP Marco Chilya ameeleza hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za makao makuu ya polisi mkoani Ruvuma.
Kamanda Chilya ameeleza kuwa watuhumiwa hao walikamatwa tarehe 18 Agosti 2025 katika Kijiji cha Mgazini Kata ya Peramiho, iliyopo Songea Vijijini na Kata ya Shauri Tanga iliyopo Manispaa ya Songea ikiwa ni muendelezo wa operesheni zinazoendeshwa na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Jeshi la Uhifadhi wa Wanyamapori (TAWA).
Kamanda ameongeza kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kuwasaka watu wote wanaojihusisha na biashara na uwindaji haramu wa wanyamapori katika hifadhi za Mkoa wa Ruvuma huku watuhumiwa waliokamatwa wakitarajiwa kufikishwa mahakamani kwa hatua za kisheria.
Katika hatua nyingine Kamanda Chilya amebainisha kuwa Jeshi la Polisi limefanikiwa kumkamata mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Maiko Lusekelo Mwakikuyu (50) kwa tuhuma za kutengeneza bidhaa bandia.
Ameeleza kuwa Mtuhumiwa huyo alikamatwa tarehe 15 Agosti 2025 maeneo ya Mjimwema, Manispaa ya Songea akiwa na pombe haramu zilizotengenezwa bila kibali ikiwemo chupa 8 za Master Portable Spirit, chupa 9 za Konyagi na chupa 3 za Smart Gin na pia alikutwa na vifaa vya utengenezaji pombe hizo vikiwemo kemikali na lebo za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Kamanda Chilya amesema mtuhumiwa huyo alikuwa akitengeneza pombe hizo haramu ndani ya nyumba aliyokuwa amepanga.
katika tukio la Tatu, Jeshi la Polisi limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa wa mauaji ya Ramadhan Hakim (19) maarufu kwa jina la Mapunda ambaye alikuwa dereva bodaboda na mkazi wa Mateka.
Kamanda Chilya ameeleza kuwa Marehemu aliuawa tarehe 19 Juni 2025 baada ya kupigwa kichwani na kitu kizito na watu wasiojulikana waliomnyang’anya pikipiki yake.
Amebainisha kuwa tarehe 15 Agosti 2025 Polisi walimkamata mmoja wa watuhumiwa wa tukio hilo Damas Atanas (32) katika nyumba ya kulala wageni T-Junction iliyopo Manispaa ya Songea na baada ya kuhojiwa mtuhumiwa alikiri kushiriki mauaji hayo kwa kushirikiana na mwenzake anayefahamika kwa jina la Erick Kifaru.
Aidha, upelelezi uliendelea na mnamo tarehe 17 Agosti 2025 Jeshi la Polisi lilifanikiwa kumkamata Erick Kifaru katika Kijiji cha Kiwanga, Bagamoyo mkoa wa Pwani akiwa na pikipiki waliyoiiba, ambayo tayari ilikuwa imebadilishwa namba za usajili.
Katika tukio la nne kamanda ameeleza mnamo tarehe 13/8/2025 Lituhi wilayani nyas, Anisia Piji(30) alijeruhiwa kwa kung'atwa meno mdomo wa chini hadi kunyofolewa Kipande cha mdomo cha chini na mtuhumiwa aliyefahamika kama mazura jina maaarufu kama Mama Yusta aliyetoroka badaa ya kutenda tukio ilo chanzo kikiwa ni ugomvi ulitokea baada ya mtoto wa mazura kupigwa na mtuhumiwa na juhudi za kumkamata zinaendelea
kamanda Chilya amesisitiza kuwa Jeshi la Polisi mkoa wa Ruvuma linaendelea kutoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za uharifu na wahalifu Ili waweze kukamatwa na mkoa Kuendelea kuwa salama wakati wote
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.